Afisa polisi wa barabarani akumbwa na kashfa nzito...Taarifa kamili hii hapa

Afisa Polisi Kikosi cha Usalama barabarani kituo cha Ubungo-jijini Dar es Salaam, Inspekta Kamote, anadaiwa kusababisha kupotea katika mazingira ya kutatanisha mkazi wa Makuburi mtaa Mwongozo, Haeshi Mohamed (59).
Kwa mujibu wa familia ya Mohamed, mzazi wao ambaye pia ni dereva wa pikipiki ya miguu mitatu (Bajaj) eneo la Ubungo, amekuwa akiandamwa na Insp. Kamote tangu Machi 7 mwaka huu, alipokamatwa kwa kosa la kuegesha pikipiki yake eneo lisiloruhusiwa.
Familia inasema “tanashangazwa na hatua ya Insp. Kamote kufika nyumbani kwetu mara mbili saa saba usiku akiwa na askari wenzake bila kuongozana na mwenyekiti wa mtaa na kudai kwamba wanamsaka baba”.

“Tuhuma ambazo tunaelezwa ni kwamba Bajaj ya baba ilioneshwa kwenye kituo cha runinga cha TBC1, ambapo mmiliki wake anadaiwa kutafuwa kwa wizi…mara wanasema baba ametishia kumroga na kumuua Insp. Kamote,” wanasema.
Mmoja wa wanafamilia, Ali Salum Kautipe, ameiambia Online kwamba mpaka sasa wanamtafuta baba yao mzazi, hawajui alipo na hawana uhakika kama amekamatwa na polisi au amekufa.

“Inashangaza Insp. Kamote kudai kwamba bajaj ya baba ni mali ya wizi. Hii ni mali halali aliyoinunua mama yetu mzazi, Zaina Ali Kapenda baada ya kuuza shamba lake la urithi wa baba yake.
“Hii Bajaj nilianza kuiendesha mimi na katika kumuenzi babu yetu ndipo nikaamua kuiandika kwa mbele “babu Kapenda”, halafu nikamwachia baba awe anaifanyia biashara…sasa leo inakuwaje mali ya wizi,” amehoji Ali.

Akisimulia chimbuko la mzozo huo, Ali amesema kuwa baada ya baba yake kukamatwa Machi 7 kwa kosa la maegesho, aliwekwa mahabusu kituo cha Ubungo kuanzia saa 9 alasiri mpaka saa 7 usiku alipodhaminiwa.

Amesema kuwa licha ya baba yake kuwa maarufu kwa askari polisi akiwemo Insp. Kamote kutokana na kuwa kiongozi wa waendesha Bajaj eneo la Ubungo, bado dhamana yake ilikuwa ya kutatanisha kutokana na mizengwe aliyowekewa.

“Baada ya kumdhamini usiku ule alikuwa akilalamika sana maumivu kwenye mbavu zake, akidai alipigwa sana. Kesho yake Machi 8, aliripoti polisi Ubungo na kuomba fomu ya matibabu (PF.3) lakini akanyimwa.

“Kwa kuwa hali yake haikuwa nzuri, tuliamua kwenda kituo kingine cha polisi Mwongozo ambapo alipatiwa PF.3 kisha tukampeleka Hospitali ya Sinza ambapo aipewa dawa na kutakiwa kurudi kwaajili ya vipimo vya X-ray,”amesema.

Ali anaongeza kuwa Machi 9, baba yao, aliripoti kituoni Ubungo na kisha kupelekwa makamani Kinondoni ambapo alisomewa kosa la kuegesha Bajaj eneo lisiloruhusiwa . Alikiri kosa na kutakiwa kwenda jela miezi minne au kulipa faini ya sh. 20,000.

Online imeona stakabadhi ya malipo namba 3416838 iliyotolewa na Mahakama ya Kinondoni kuthibitisha kwamba Mohamed alilipa faini hiyo na kuachiwa huru na baadaye alikabidhiwa Bajaj yake iliyokuwa ikishikilia kituoni Ubungo.

Ali anasema, “tukiwa kituoni kabla ya kwenda mahakamani, Insp. Kamote alimnyang’anya baba vielelezo vyake vya matibabu ili asiweze kurejea tena hospitali kwa ajili ya vipimo”.

Familia hiyo inadai kuwa baada ya siku mbili kupita tangu kumalizika kwa kesi hiyo, ndipo usiku wa saa saba walivamiwa na askari polisi wakiongozwa na Insp. Kamote wakidai kumsaka baba yao kwa tuhuma za kutishia kumroga na kumuua afisa huyo.
“Kwanza tulishtuka sana kuona askari wanakuja kupekua nyumba yetu kumtafuta baba bila ya kuongozana na mwenyekiti wa mtaa kama ilivyotaratibu za utawala bora… walipekua kila mahala na kuwabughudhi wapangaji wetu.

Insp. Kamote aliingia hadi chumbani kwangu nikiwa nimelala na mke wangu, akawasha taa na kuizima,” amesema.
Familia inaongeza kuwa tukio hilo la kuvamia mara mbili na askari usiku kisha kupekuliwa, limewafanya wapangaji wao kutaka kuhama kwani wanahofia wanaweza kukamatwa.

“Tangu askari walipofika hapa siku ya kwanza, baba yetu hakuonekana tena hadi leo, hatujui kama walimkamata au kapotea na kufa…maana bado tunaambiwa anatafutwa,”wamesema.
Alipoulizwa Insp. Kamote kuhusu tuhuma hizo, alikiri kutafutwa kwa Mohamed akisema, “ameunda genge na wenzake na kunitisha kwamba wataniroga na kuniua, kwa hiyo bado tunawatafuta”.

Online liliotaka kujua taratibu za kisheria kama zinaruhusu kwa yeye mlalamikaji kufanya tena kazi ya ukamataji wa mtuhumiwa, Insp. Kamote aling’aka na kusema, “sina muda wa kuongea na wewe…wewe nani unaifundisha polisi kazi”, kisha akakata simu.

Baada ya dakia mbili alipiga tena na kumtaka mwandishi amfuate ofisini kwake ili ampatie majibu, lakini alipotakiwa kuyatoa kwa njia hiyo ya simu, akasema, “una ajenda yako, andika munavyoona…wewe raia unaweza kumhoji polisi, unataka kutufundisha kazi”.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wabura, alipoulizwa kuhusu sakata hilo amesema, “mwambie huyo anayelalamika afike kwangu ndipo naweza kufanya uchunguzi”.

Ameongeza kuwa kwa sasa itakuwa vigumu kwake kulitolea taarifa halisi na za uhakika ikiwa hajapata malalamiko ya wanafamilia hao.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright RAHA TAMU Published.. Blogger
Back To Top